Jumamosi. 18 Mei. 2024

Mt. William wa Burge, Askofu

William wa Burge, Askofu

Tangu utoto wake, William alimwelekea Mungu. Aliingia Upadre, akamtamani Mungu zaidi na zaidi. Kwa nia hiyo ndipo akakusudia kujitenga na malimwengu. Mwisho alijiunga na Mamonaki, akaishi kitakatifu. Alikuwa mpole, mkunjufu, na mwenye kicheko usoni kwa mamonaki wenzake.

Baada ya muda akafarikia Askofu wa Burge (Bourges, Ufaransa). Basi, mapadre wa huko hawakujua wamchague nani badala ya Askofu huyo. Wakapeleka habari kwa Askofu wa Paris, ndugu ya Askofu aliyefariki, kumwomba shauri lake. Wakampelekea mapadre watatu, William akawa mmoja wao. Askofu akaamuru majina hayo yaandikwe katika vyeti vitatu mbali mbali, vikunjwe na viwekwe altareni wakati wa Misa. Kisha Misa Askofu akatwaa cheti kimoja, ambacho kilikuwa kimeandikwa jina la William. Basi, watu wakaona Mungu amemchagua awe Askofu wa Burje.

William akalisimamia jimbo hilo kwa nguvu zake zote, akitumia pia upole hata akalistawisha sana. Kisha kufa, maiti yake ilizikwa katika kanisa la Burje. Miujiza mingi ilitendeka kwenye kaburi lake, hata mwishowe Papa akamtaja kuwa Mtakatifu mwaka 1218.

Maoni


Ingia utoe maoni