Jumapili. 08 Septemba. 2024

Tafakari

Jumapili, Septemba 25, 2016

Jumapili, Septemba 25, 2016.
Dominika ya 26 ya Mwaka


Amo 6: 1, 4-7
Zab 146: 7-10
1 Tim 6:11-16
Lk 16: 19-31


MATOKEO YA YESU!

Leo katika Injili ya Luka tunakutana na mfano wa tajiri na Lazaro. Mfano huu una sehemu mbili, sehemu ya kwanza ni maisha ya hapa duniani na sehemu ya pili ni maisha yajayo baada ya maisha ya duniani. Kuna mgongano wa tofauti kati ya sehemu hizi mbili zinapo linganishwa. Katika sehemu ya kwanza tajiri ana chakula kizuri na Lazaro ana njaa, na sehemu ya pili Lazaro yupo na Abraham na tajiri anateseka na kupata kiu.

Inaogopesha na kutisha kusikia matokeo ya huyu tajiri katika maisha yajayo. Huyu tajiri hakufanya chochote kibaya, hakudanganya, au hakuiba chochote cha Lazaro. Sasa kwa nini apate adhabu kubwa namna hio? Kujibu hili swali, ni lazima na kwanza kabisa kujua kuna aina mbili za kutenda dhambi-ya kwanza, kutenda au kuamuru ili itendeke na pili kutokutimiza wajibu. Sisi tunajua dhambi za kutenda, kwa mfano kuiba, kusema uongo, kuiba nk. Kwa upande mwingine tunatenda dhambi kwa kutotimiza wajibu, na mfano mzuri wa dhambi ya kutotimiza wajibu ni mfano wa leo kutoka katika Injili. Huyu tajiri haku adhibiwa kwasababu alitenda kitu fulani, bali hakutimiza wajibu aliopaswa kutenda. Maskini Lazaro alikuwa katika mlango wake akiteseka na njaa na kuugua. Kwa hakika lazima huyu tajiri alikuwa akimuona kila wakati alipo ingia nyumbani mwake lakini hakuna hata siku moja alifikiria kumsaidia au angalao kumpa kitu cha kula hata angalao angempa mabaki ya chakula, hii ni kwasababu maskini Lazaro alikuwa tayari kula hata mabaki yaliyo dondoka katika meza yake. Tajiri huyu alishindwa kushirikisha utajiri wake hapa duaniani na hivyo anakosa kushirikishwa utajiri wa maisha yajayo.

Hali hiyo hiyo inaonekana katika somo la kwanza kutoka katika kitabu cha Amosi. Bwana anatoa ujumbe mdogo unao onesha kukuwa kwa tofauti kati ya matajiri na masikini. Hali ya uchumi ya Israeli kipindi cha Amosi ilikuwa imekuwa na kusitawi kama katika hali ya yule tajiri katika mfano wa Injili na maskini walikuwa maskini kweli kweli, katika hali ya kutisha kabisa. Mungu anawaka hasira yake kusema ‘Ole wao wanaostarehe’ wakati maskini na wahitaji wanateseka kwa njaa, wakati matajiri wana karamu zao za kondoo walio nona, divai, ninyi mnaolala juu ya vitanda vya pembe. Mungu hakasiriki kwasababu wanafurahia ni kwasababu wamesahau kuwajali masikini na kuwa shirikisha wahitaji wanao teseka kwa umaskini na njaa.

Ndugu zangu kuwa tajiri sio kitu kiovu bali uovu nikuwa mchoyo, mbinafsi na usiyejali. Kanisa katika maandiko yake kuhusu mtizamo wa jamii inaongelea kuhusu lengo la rasili mali ya duniani. Kwa kufafanua kwa urahisi zaidi ni kwamba, wakati mtu akiwa na kitu/vitu vingi mno hata asivyo hitaji anakuwa amechukua sehemu ya mwingine anaye hitaji. Ukiukwaji wa mtizamo huu wa Kanisa, unakuwa unapinga wema ambao unapaswa kutendwa na hapo dhambi nyingi za kutotimiza wajibu huwa nyingi. Hali hii tunaiita “KISA CHA LAZARO NA TAJIRI”.
Katika hali ya sasa, tunakutana na “KISA CHA LAZARO NA TAJIRI”. Kila mahali katika ulimwengu; tuna nchi kubwa zilizo endelea walio hifadhi chakula ambacho hata hawajui watatumia lini tofauti na Nchi maskini ambapo watu wake wana hangaika kila siku kupata mlo wa siku. Kuna majengo makubwa tena marefu katika miji yetu ya nchi zetu ambapo watu huishi maisha ya kifahari tofauti na watu wanaoshi katika hali ngumu tena bila kuwa na uhakika wakupata chakula au mlo wa siku.

Kuna tofauti nyingi ambazo tunaweza kuoanisha katika maisha na leo Yesu anatuita tuweze kuondoa tofauti hizi katika maisha yetu na tuishi kwa upendo, kujaliana na usawa. Mt. Teresa wa Kalkata alisema “Kwa kidogo zaidi tulicho nacho ndivyo tunavyozidi kutoa zaidi, inaonekana kama ujinga lakini ndio mantiki ya upendo”. Aliguswa na MATOKEO YA YESU, kutafuta Amani, furaha na upendo kwa kuwa na kidogo na kwakutumia hicho kidogo kuwashirikisha wengine. Je, tunaweza kuchukua mfano wake kwa kuguswa na ujumbe wa Injili, kwa MATOKEO YA YESU na kuleta ufalme wa Mungu kati yetu. Matokeo ya Yesu maana yake, Yesu akigusa maisha yako na ukabaki mwaminifu kadiri ya mafundisho yake, matokeo yake ni kufurahi naye katika Maisha yajayo.

Sala: Bwana Yesu, fungua macho yetu tuweze kuona mateso ya ndugu zetu wanao tuzunguka na utupe nguvu ya kushirikishana nao yale ulio tujalia, ili nawao waweze kuhisi upendo wako kwa kupitia sisi. Amina

Maoni


Ingia utoe maoni