Ijumaa. 18 Oktoba. 2024

Tafakari

Jumapili, Septemba 11, 2016

Jumapili, Septemba 11, 2016.
Dominika ya 24 ya Mwaka C wa Kanisa

Kut: 32:7-11.13-14
Zab 51: 1-2.10-11.15.17
1Tim 1:12-17
Lk 15: 1-31

URAFIKI NA MUNGU!

Katika somo la kwanza kutoka katika kitabu cha Kutoka, tunasikia mazungumzo kati ya Mungu na Musa. Mungu ana hasira lakini Musa anajaribu kupooza hasira ya Mungu. Watu wazamani walitambua kuwa Mungu aliwapenda, kwahiyo walitegemea Mungu atakasirika wakati watu watakapofanya vitu ambavyo hamna rafiki anayeweza kufanya. Musa alikasirika kwasababu watu aliowashughulikia namna hiyo kwa nguvu zake zote hawakujali. Musa hakuweza kuamini kwamba baada ya yeye kugeuza mgogo tu, wao walianza kujitengenezea ndama ya shaba kama kimungu chao, alama inayoonesha waliiga miungu ya Wakanaani. Musa alifikiria “Kama mimi nikikasirika, Mungu atakuwa zaidi, sasa nitawezaje kumuomba Mungu asiwaangamize?”

Kama rafiki, Musa anakuwa katikati ya Mungu na watu wadhambi. Anamuomba Mungu akumbuke kwamba sio kila mmoja atakuwa amejihusisha na udhaifu huo. Anamkumbusha Mungu kwamba Mungu ana marafiki waaminifu walio na shukrani kwakulindwa na kuongozwa jangwani. Na kama rafiki mwema Musa anaenda zaidi kumkumbusha Mungu kwamba atafanya uharibifu, Mungu atapoteza uso wake. Simulizi hili linaishia Mungu anaamua kuwasamehe watu wake.

Ni simulizi la hali ya juu kabisa! Linatuonesha ni kwa jinsi ghani wazee wetu walivyojiona wenyewe katika mahusiano na Mungu. Musa alijiona mwenyewe, sio kama mtoto wa Mungu, bali kama anayeshirikiana naye, rafiki wa Mungu. Wakati watu walivyo muangalia Musa walitambua anamchukulia rafiki yake katika hali ya juu kabisa, wakaanza kujifunza kutoka kwake.

Wakati watu walivyokutana na Yesu, walitambua pia urafiki wake wa karibu na Mungu. Kwa hakika walikuja kutambua kwamba Mungu Baba na Yesu walikuwa karibu zaidi ya rafiki. Yesu kama Musa, aliwatia moyo watambue kuwa urafiki na Mungu ni kitu ambacho kipo kwa ajili ya wote. Katika Injili tunamsikia Yesu akimuelezea Mungu katika katika hali ya kufariji sana. Kwanza kama mkulima anayetunza kondoo wake na anafanya kazi ngumu kabisa kwa ajili ya usalama wao. Anamuita Mungu pia kama Mama wa nyumbani aliye huzunika kwasababu ya kupotea kwa kiasi kidogo tu cha fedha na anaitafuta mpaka aipate. Tunapopotea Mungu hatuachi anatutafuta daima. Furaha ya Mungu tuunganike naye daima, yeye hafurahii kifo cha mtu muovu, anapenda tutubu ili turudi kwake.

Tuwe tayari kutengeneza tena urafiki wetu na Mungu. Mwenye kushika maagizo ya Mungu ana Amani ya kweli. Maisha ya dhambi hayana raha na wala huwezi kuwa na uhuru wa kweli. Tuepuke kitu chochote ambacho chaweza kuwa kimungu chetu, ambacho kinabomoa urafiki wetu na Mungu. Ingekuwa vyema sana leo kuamua kutoka moyoni kabisa na kumuomba Mungu atusaidie tuweze kujenga tena urafiki mpya kabisaa. Tusiridhike na dhambi zetu, wala tusiwe kama watu wanaosikia maneno ya Mungu na kuyasahau. Siku ya dominika ya leo, tuchukue angalao haya tu, kujenga tena upya urafiki wetu na Mungu. Urafiki wa kweli na Mungu ni furaha ya moyo na matumaini ya furaha ijayo.

Musa alionesha mfano mzuri kwa kuwaombea ndugu zake waliokuwa wadhmbi. Pengine tujaribu kujiuliza ndugu yangu anavyokosa najaribu kumuombea kwa Mungu ili abadilike? Au ndio tunapata muda wa kukaa chini na kuanza kumsema na kumshindilia chini kabisa? Tuna mazoea ya kuomba kwaajili ya mazuri ya wenzetu? Ninapenda kutumia mfano huu kila mara kwamba “hata jani la mwisho kabisa kwenye mti ni sehemu ya mti”, mkristo anayeonekana ni mdhambi kabisa na hafai machoni petu bado ni sehemu ya mwili wa Kristo. Kama Musa tumuombee ili aweze kuguswa na neema ya Mungu nakuwa mwema tena, nakuendelea kufurahia ufuasi wake ndani ya Kristo. Hakuna asiyefaa machoni pa Mungu, hata yule adui yako mkubwa kabisa unayedhani huwezi kumsamehe bado ni sehemu ya mwili wa Kristo.

Je, tunamuona Mungu kama rafiki wa kweli, ambaye kila kitu chetu ni kutoka kwake? Tukimuona Mungu katika hali hii, tutajitahidi kila wakati kuwa waaminifu katika urafiki huu. Tumuombe Mungu Roho Mtakatifu atuunganishe kila wakati katika mapendo na urafiki wetu na Mungu daima.

Sala: Bwana Yesu, nakushukuru kwa kuwa rafiki yangu. Ninakuomba pia niwe mwaminifu kwa urafiki huu. Amina.

Maoni


Ingia utoe maoni