Alhamisi. 16 Mei. 2024

Tafakari

Ijumaa, Juni 30, 2017

Ijumaa, Juni 30, 2017,
Juma la 12 la Mwaka

Kumbukumbu ya Wafiadini wa Kwanza wa Kanisa la Roma

Mwa 17: 1, 9-10, 15-22;
Zab 128: 1-5;
Mt 8: 1-4


KUWA KAMA KRISTO KATIKA KUPENDA NA HURUMA

Katika somo la Injili Yesu anatenda kisicho fikirika. Anamgusa “mkoma” ambae hapaswi kuguswa. Wakoma walikuwa watu wasio thaminika kabisa na kutengwa katika jamii ya Wayahudi. Hawakuwa wametengwa tu bali walikuwa wanachukuliwa kama “wameshakufa tayari”! hata na ndugu zao. Sheria za Kiyahudi zilikataza mtu yeyote kusogelea mkoma au kumgusa, kwani atatiwa najisi. Akitambua hili, mkoma kwa kushangaza anamkaribia Yesu kwa ujasiri na unyenyekevu, akitazamia uponyaji kutoka kwa Yesu. Yesu hakumpa tu huyu mkoma kile alichokuwa akihitaji bali anaonesha upendo na huruma na ukarimu wa Kimungu kwa kumgusa. Anaonesha upendo na huruma ya Kimungu katika hali ya kugusa zaidi badala ya maneno matupu. Alimgusa mkoma na anamfanya awe safi tena-sio kimwili tu bali pia kiroho. Matokeo yake ni kwamba alirudishiwa tena afya yake na kuwa mzima kabisa.

Yesu alimpenda huyu mkoma alipenda kumpa zawadi yake ya thamani ya uponyaji. Alifanya haya kwa huruma, na alihitaji ashukuru. Hakupenda kufanya hili hadharani. Sisi nasi tunapaswa kuiga hilo. Tunapaswa kutambua kuwa Mungu anatupenda sana kiasi kwamba anataka kutunyanyua juu kutoka katika mizigo yetu na kutuponya kutoka katika madhaifu yetu kwasababu tu, anatupenda.

Tutafakari leo, juu ya kinacho sababisha sisi tuwe na ukarimu kwa watu. Tuombe ili nasi tuweze kufanya katika hali ambayo haitafuti heshima ili tuweze kuiga tabia za Kimungu.

Sala: Bwana, ninaomba nikuwe katika mapendo kwa wengine na nioneshe mapendo hayo katika hali ya ukamilifu wako. Ninaomba nisivutwe na tamaa ya kusifiwa. Yesu nakuamini wewe. Amina.

Maoni


Ingia utoe maoni