Alhamisi. 16 Mei. 2024

Tafakari

Jumatano, Juni 14, 2017

Jumatano, Juni 14, 2017
Juma la 10 la Mwaka

2 Kor 3: 4-11;
Zab 99: 5-9;
Mt 5: 17-19.


SHERIA YA UPENDO!

Katika Injili ya leo, Yesu kwa hakika anawahakikishia wanaomsikiliza kwamba, “Sikuja kutengua sheria na manabii. Nimekuja si kutengua bali kuikamilisha”. Yesu alikuja si kuifuta sheria bali aiinue katika hali ya juu ya ukamilifu. Mtazamo wa Yesu unatusaidia tuione sheria katika mwanga mpya. Maneno yake ni kwa ajili ya kufariji lakini pia yanaleta changamoto, akionesha njia inayoenda juu sana kuliko sheria mpaka kwenye sheria ya Upendo. Sheria isiyo na upendo haiwezi kulinda utu na maisha ya mwanadamu. Inamfanya mwanadamu awe kama aina fulani ya kitu kisicho na uhai. Yesu anatutaka tuwe na upendo zaidi. Pengine wakati mwingine tunasisitiza mno sheria kiasi cha kushindwa kuonesha upendo na msamaha kwa wengine.

Tuwatazame watu walio wekwa na Mungu mbele yetu ili tuwapende. Hili ni kwa ajili pia ya ndugu zetu katika familia lakini pia katika wana ndoa. Je, ni mara ngapi tunavyokuwa makini kwa kitendo kidogo cha huruma na upendo?. Je tunatafuta muda wa kutumia maneno ya kutia moyo? Je, tunatumia jitihada hata kuwaonesha kwamba tunawajali? Upendo upo katika utukufu na utukufu huu unaonesha kushika amri ya Mungu ya mapendo.

Katika maisha yetu, tunapaswa kuwa tayari kusonga mbele tukiwa wabunifu wa njia mpya za kuweza kutufanya tuelewe na kuishi Imani yetu zaidi. Tamaduni zetu na mapokeo yetu ni mazuri na tusiyapoteze lakini pia tutumie hali hiyo hiyo katika kuelewa na kuangalia hitaji la sasa.

Sala: Bwana, nisaidie niweze kuwa makini kwa njia kubwa na katika njia ndogo ndogo unazo niita ili kukupenda wewe na jirani. Nisaidie hasa, niweze kuangalia muda hata mdogo nioneshe upendo na hivyo kutimiza sheria yako. Yesu nakuamini wewe. Amina.

Maoni


Ingia utoe maoni