Alhamisi. 16 Mei. 2024

Tafakari

Alhamisi, Juni 08, 2017

Alhamisi, Juni 8, 2017.
Juma la 9 la Mwaka

Tob 6:10-11, 7:1, 9-14, 18:4-9;
Zab 127: 1-5;
Mk 12: 28-34.


PENDA KAMA UNAVYOPENDWA NA MUNGU!

Kwakusoma Injili tunaweza kufanya muktasari wa nafsi ya Yesu kwa neno moja tu, nalo ni UPENDO. Yesu anatuambia kwamba sheria zote zinaweza kufupishwa katika sheria mbili tuu. Ya kwanza kabisa ambayo ni muhimu sana ni upendo kwa Mungu usio na masharti, ya pili ni matokea ya hiyo ya kwanza, kwasababu wakati mwanadamu anapendwa, Mungu anapendwa, kwasababu mwanadamu ameumwa kwa sura na mfano wa Mungu

Upendo ulimsukuma Yesu aweze kuwanyanyua wanyonge, kuwasaida waliotengwa, kuponya walioumizwa, kuwafanya huru wafungwa na akatoa maisha yake msalabani ili kutukomboa sisi kutoka utumwa wa dhambi. Upendo wa Mungu hauna masharti. Yesu kwa maneno na matendo yake anatuhimiza kutimiza na kutenda “UPENDO huu” kwaajili ya ukombozi wetu na ukombozi wa ulimwengu mzima. Na hiki ndicho kitambulisho chetu kama Wakristo wanaomfuata Yesu kwa uaminifu. Kwa namna hiyo tutakuwa Wakristu wa kweli “kama Kristo”. Pengine tujiulize swali lingine ambalo hatujazoea sana kujiuliza, tunajua Mungu anatupenda wote bila ubaguzi. Je, ninampenda mwenzangu/jirani yangu kama Mungu anavyompenda?

Kumpenda Mungu ni kitu cha muhimu kabisa tunacho weza kufanya na hivyo ni ufunguo wa kujipenda sisi wenyewe. Kumpenda jirani kama nafsi zetu maana yake kila tunachofanya kinapaswa kimsaidie mtu kuweza kumpenda Mungu zaidi kwa moyo wote, akili zote na nguvu zote. Haya yanafanywa na maneno yetu lakini zaidi kwa misaada yetu kwao. Tukimpenda Mungu kwa kila kitu, upendo wetu kwa Mungu unakuwa unasambaa kwa wengine. Wengine wataona upendo wetu kwa Mungu, tamaa yetu kwa Mungu na majitoleo yetu kwa Mungu. Wataona na kuvutwa. Kwa kutoa ushuhuda huu wa upendo unakuwa kivutio kwa wengine kumfuata Mungu.

Sala: Bwana, nisaidie niweze kufuata amri hii ya mapendo. Nisaidie nikupende wewe kwa jinsi nilivyo bila kubakiza kitu. Na katika mapendo haya yako, nisaidie kushirikisha wengine. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Maoni


Ingia utoe maoni