Alhamisi. 16 Mei. 2024

Tafakari

Jumanne, Mei 09, 2017

Jumanne, Mei 9, 2017,
Juma la 4 la Pasaka.

Mdo 11:19-26;
Zab 87:1-7 (R. 117:1);
Yn 10:22-30.


IMANI NI LUGHA YA KUMFAHAMU MUNGU!

Katika somo la kwanza Barnaba anaona Roho Mtakatifu akifanya kazi ndani ya watu wa Antokia na hivyo anawatia moyo na kuwapa nguvu “Wakristo”. Katika somo la Injili, Wayahudi wanakataa kumkaribishi Yesu. Wanamuuliza “kama wewe ni Kristo tueleze wazi”. Na Yesu anajibu kwamba, “nime waambia lakini hamkusadiki”. Je wewe unasadiki Yesu ni nani kwetu? Je tupo wazi kwa kazi ya Roho Mtakatifu?

Pengine umemtaka Mungu ashuke kutoka mbinguni aje akupe majibu wazi ya kwanini baadhi ya mambo yapo kama yalivyo au kama yanavyo tokea? Au kukupa majibu wazi ya maswali yako. Lakini hafanyi hivyo. Anafanya hivyo katika hali ya njia yake kamili kwa lugha yake kamili. Ni kwa lugha ya Imani na hii inahitaji kujikabidhi kwa Mungu kabisa na mapenzi yetu yote ili tuweze kusikia na kuelewa. Hii ndio njia ya kweli ya kuongoka na kuwa katika njia ambayo Mungu anataka sisi tuwe. Tukitegemea akili na utashi wetu wenyewe, tutashindwa kuona uwepo wa Mungu, na kama tutataka akili yetu itoe majibu yote, ni wazi kwamba tutafikia mahali pakuona hamna haja ya Mungu kwasababu tunajitosheleza kwa akili zetu. Imani yaweza kutupa majibu ambayo akili zetu haziwezi kutambua.

Sala: Bwana, mara nyingi nimeshindwa kukusikiliza wewe na kukuelewa kwa njia ya zawadi ya Imani. Mara nyingi nimependa kupata majibu marahisi kwa maswali magumu. Nisaidie niweze kukuwa katika uvumilifu ili niweze kukufahamu na kukuruhusu kuwa Mchungaji wangu. Yesu nakuamini wewe. Amina

Maoni


Ingia utoe maoni