Ijumaa. 18 Oktoba. 2024

Tafakari

Jumamosi, Mei 25, 2024

Jumamosi, Mei, 25 2024,
Juma la 7 la Mwaka wa Kanisa!

Yak 5: 13-20;
Zab 141: 1-3, 8;
Mk 10: 13-16


WATOTO WA UFALME WA MUNGU!


Yesu anatuambia leo ufalme wa Mungu nikwawale wanaoukaribisha kama watoto. Nini maana yakuwa kama mtoto?

Watoto ni Wanyenyekevu. Matendo ya watoto ni ya asili, ni wawazi, waaminifu, na wapo huru bila hatia katika kutenda na kuongea. Vijana na watu wazima wamepoteza fadhila hizi, katika hali ya kujijengea jina, ufahari, madaraka na heshima.

Watoto ni watii. Watoto ni watii kwa wazazi wao. Ingawaje tunawaona watoto wengi wasio tii lakini hata hivyo wanamfikiria mzazi zaidi kuliko mtu wa nje. Wapo tayari kufuata lililo zuri, bila hata kubisha. Lakini sisi ni watii kwa nafsi zetu tuu, tunachosema, ninachofikiri ndio njia sahihi.

Watoto ni Tegemezi. Watoto wanatambua hawajiwezi, kwahiyo wanategemea walimu, wazazi, ndugu na walezi. Wanajiamini na hawana wasi wasi. Kama ulishawahi kumvusha mtoto barabara hii kwenda nyingine unaweza kutambua ni jinsi ghani anavyo jiamini anakushikilia mkono bila kuachia. Hata Imani yao juu ya Mungu. Kila wanachojifunza kuhusu Mungu, wanakishikilia kwa Imani na kujiamini. Je, sisi tunamshikilia nani mkono atuvushe salama. Ulishawahi kutambua ukiwa umeungama na umejipatanisha na Mungu na wanadamu unavyopata furaha na kujianmini moyoni? Bado unaendelea kushikilia dhambi zako? Mpaka lini?

Watoto wanasahau. Watoto hawabebi vinyongo na malalamiko na machungu. Wakati wametendewa vibaya wanasahau haraka, na kwasababu wanasahau haraka hawana hata muda wakusamehe, kwasababu watasameheje kitu wasichokumbuka? Hili kwetu sisi ni ngumu sana, hatutaki kusahau wala hatutaki kusamehe? Mpaka lini ndugu?

Watoto hawasitisiti. Kitu cha pekee katika watoto, hawana mwisho katika kuongea, kuuliza wala kukupatia kitu Fulani. Watakuuliza kila kitu kuanzia chocolate mpaka ndege. Pia wanashirikisha kile kidogo alichojifunza. Pia wataongea kuhusu kitu chochote alichoona nakusikia. Je, sisi tupo kama watoto, tuna muda wakuongea na Mungu? Je, tunakuwa na muda wakumuomba kitu? Je, tunashirikisha wengine alichotujalia Mungu.

Sasa leo, tunaitwa tuwe kama watoto wachanga, tufanane na watoto wachanga. Ni wakati pia wakuwazuia watoto wasijiingize sana kwenye mambo ya mtandao, simu, na mambo mengine ambayo yatawafanya wapoteze ile thamani yao kama watoto. Siku hizi tuna simu zenye michezo ambayo inafundisha jinsi ya kupigana vita, katuni zisizo na mafundisho mazuri, zenye kufundisha uchoyo na mengine. Je tupo tayari kulinda ile roho ya uaminifu ya watoto?

Sala:
Bwana, fanya mioyo yetu iwe kama ya watoto. Bariki na linda uaminifu wa watoto wetu.
Amina.

Maoni


Ingia utoe maoni