Jumamosi. 18 Mei. 2024

Tafakari

Jumamosi, Oktoba 28, 2023

Jumamosi, Oktoba 28, 2023
Juma la 29 la Mwaka

Sikukuu ya Wat. Simon na Yuda

Efe 2: 19-22;
Zab 19: 1-4 (R) 4;
Lk 6: 12-16.

TUMITWA TUWE WAKAMILIFU!

“Mungu hawaiti walio wakamilifu bali Mungu ndiye anaye wakamilisha walioitwa”. Maneno haya ya Mungu yananifanya mimi nifikiri ni kwa jinsi gani njia za Mungu ni tofauti kabisa na mtazamo wa ulimwengu. Kwa kazi zote nzuri, ili kupokelewa katika shule Fulani nzuri, kwa viongozi nk. Mara nyingi tunaangalia na kuchagua wale walio wazuri, wale wenye ujuzi na maarifa makubwa. Yesu aliwachagua watu wa kawaida kabisa kuwa Wafuasi wake na mabalozi kwa mataifa yote. Yesu anatufanya sisi tusahili pia, anatufanya sisi tustahili sisi ambao ni wepesi kuvunjika kama chombo cha mfinyazi ili kuwa “sehemu ya Roho wa Mungu anamo kaa” (Ef 2: 22). Anatufanya sisi mashahidi wa neno lake mpaka miisho ya ulimwengu. Anatupa sisi nguvu ya kudhihirisha ufalme wa Mungu ulimwenguni kwa kuwaletea watu uponya wa roho na kufunguliwa katika vifungo vya dhambi.

Mungu humwalika mwanadamu daima katika kazi yake ya ukombozi. Yesu aliwachagua watu wa kawaida kabisa wa kipindi chake kuwa mitume wake. Anawapa nguvu na mamlaka na wakawa waaminifu katika kuendeleza kutimiza mapenzi ya Baba. Luka, anatuambia Yesu alienda mlimani kusali, na alikesha usiku kucha katika kusali. Ndipo baada ya kusali anawachagua mitume kumi na mbili. Na kati ya hao wawili ndio tunafanya sikukuu yao leo, Simoni na Yuda. Habari za hawa wawili zijulikanazo ni chache sana. Tunajua walichaguliwa na Yesu kuwa mitume wake. Mtume ni yule anayetumwa. Hawa walishirikiana kufanya kazi pamoja katika nchi ya Uajemi na huko waliuawa kwa ajili ya Kristo. Kwasababu hiyo sikukuu yao huadhimishwa pamoja. Mtume simoni aliitwa ‘Zeloti’ maana yake mwenye bidii kwasababu alifanya bidii kutangaza ujumbe kuhusu Yesu kokote. Mtume Yuda aliitwa ‘Tadayo’maanake ‘hodari’ili kumtofautisha na Yuda Iskarioti msaliti. Alikuwa ndugu yake Yakobo mdogo kama tunavyosoma katika Injili na kama anavyosema mwenyewe katika barua yake ‘Barua ya Yuda’na barua hii iliandikwa kwa ajili ya makanisa yaliokuwa karibu na nchi Takatifu kama alivyofanya nduguye Yakobo.

Unaweza kufikiria ni watu wa namna ghani aliokuwa nao Yesu. Petro aliyekuwa msemaji na mwenye hofu lakini bado Yesu alimchagua kuongoza. Yakobo na Yohane waliokuwa wakipigania kuwa karibu na Yesu katika ufalme walio utafsiri vibaya; Mathayo mtoza ushuru, nk. Tunaweza kufikiria kukaa kwao pamoja kulikuwa je hapo mwanzo. Pamoja na kutoelewana wao kwa wao waliponywa na upendo usiozuilika wa Yesu alioutoa kwao.

Somo la kwanza linamalizia vizuri kabisa: “tangu sasa ninyi si wageni tena wala wapitaji, bali ni wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu”. (Efe 2:19). Je, tupo tayari kumruhusu Yesu atujenge kama watu wa nyumba yake, hata ikiwa nikuwa pamoja na wale tusiowapenda?

Sala:
Bwana, nipo hapa kuyafanya mapenzi yako. Nitumie mimi kama ulivyofanya kwa watakatifu Simoni na Yuda kuwa mitume wako ulimwenguni. Yesu nakuamini wewe.
Amina

Maoni


Ingia utoe maoni