Jumatatu. 16 Septemba. 2024

Tafakari

Jumapili, Februari 05, 2017

Jumapili, Februari 5, 2017.
Dominika ya 5 ya Mwaka A wa Kanisa

Isa 58:7-10;
Zab 112: 4-9;
1Kor 2: 1-5;
Mt 5:13-16


CHUMVI NA MWANGA WA DUNIA!

Ukristo sio dini ya mtu binafsi. Ukristo ni mwanga unaokusudiwa kubadili ulimwengu, na wala hamna shaka kuhusu hilo kwamba, kwa kiasi kikubwa, umefanya hivyo. Lakini, inaonekana kwamba baadhi ya wafuasi wanafanya kama vile kucheza mchezo wa “kujificha na kutafuta”. Hawaonyeshi Imani yao au hawaishi Imani yao inavyopaswa. Wakristu wengi wanajificha kwenye kundi. Wanaficha Imani yao kwa kutembea kwenye kundi, wanashirikiana na wengine kwenye mambo ambayo sio ya muumini wa kweli. Tunapo kumbatia dunia na vipimo vyake, bila kujitambua, tunajikuta tumenaswa na Ulimwengu. Tunapo ficha Imani yetu na kuishi, kama vile tu ulimwengu unavyo ishi, ulimwengu unatupepeta unavyopenda.

Lakini pia, kama unaishi kama mwanga, ukaonyesha upendo wa Kimungu, kukubali mapenzi yake na neema zake, watu watavutwa kwako watakapo kuwa wanakumbana na giza kama vile vipepeo wanavyofuata mwanga usiku. Kuna sababu moja ya sisi kuwa mwanga na chumvi kwa wengine nani kwanjia hiyo watu waweze kuvutwa kwa Mungu kama Bwana wao. Umuhimu wetu wakuishi Injili katika hali ya juu kabisa ni ili kuwavuta watu na kuwaelekeza kwa Mungu ambaye anawapenda na ambaye ndiye furaha ya juu kabisa. Jukumu letu ni kuwaelekeza watu waishi katika Ulimwengu ambao Mungu anapenda sisi tuishi. Hili linawezekana kwa watu wote tena wa kawaida kabisa, hata wasio soma. Sio kitendo cha kuongeza akili bali kushirikishana uzoefu wetu wa kuwa na Mungu. Tukiishi kama chumvi na Mwanga, tunaleta furaha na kiburudisho, matumaini na muongozo kwa wote walio karibu yetu. Watu watatutafuta.

Chumvi ni kitu cha pekee kabisa kinacho ongeza ladha kwenye chakula. Chumvi yenyewe tu bila chakula haileti ladha sana. Lakini inapo ongezwa kwenye chakula, vyakula mbali mbali, inaingia ndani na kuleta ladha nzuri. Tunakumbushwa kuwa sisi ni “ chumvi na mwanga”. Kama chumvi, hatujaitwa kujijengea umaarufu wetu wenyewe na kuwa wabinafsi. Hatuja umbwa kwa ajili yetu wenyewe. Ni jukumu letu kama Wakristu kuingia katika Ulimwengu wetu, na kuongeza ladha, kwa kuusaidia ubadilike kuwa ulimwengu wa neema na huruma, ulio jaa “ladha” ya Ufalme wa Mungu. Hili linafanywa kwa kujenga uhusiano mwema. Hili linafanywa kwa kugusa maisha ya watu na kuwavuta kwa Kristo. Upendo wa Mungu tunaoleta ulimwenguni, na katika maisha ya wote tunao kutana nao, yataonekana dhahiri kuwa ni chumvi inaingia katika chakula na kuleta ladha.

Je, tunapotezaje ladha? Kwa maneno mengine, tunashindwaje kuwa “chumvi ya Ulimwengu?’ Tunafanya haya tunapo ingia ulimwenguni, na kushindwa kuishi maisha baada ya maisha yetu kukutana na watu mbali mbali na kushindwa kweli kugusa maisha yao.Wakati maisha yetu mbele ya wengine hayana chochote cha kuongeza au hayana ladha yoyote yakuongeza katika chakula, na hapo matendo yetu yanakuwa kama chumvi ilioisha ladha ambayo ni nzuri tu kwa kutupa na kukanywagwa na watu. Kama tunashindwa kuleta mabadiliko katika maisha ya wengine, tunakosa mwelekeo wa uhusiano na tunashindwa kuwa chumvi ya dunia.

Tutafakari juu ya hili jukumu tulilopewa na Kristo, wito tuliopewa wakuleta mabadiliko duniani katika maisha ya wengine. Watu wanapokuwa katika Imani na upendo kwasababu ya uwepo wako katika maisha yao, tunatimiza agizo la Kristo kwamba sisi ni chumvi na Mwanga wa Ulimwengu. Tujitahidi sisi wenyewe kuwa chumvi ya dunia ili ulimwengu wetu uweze kuwa sehemu nzuri ya kuishi, uliojazwa na ladha ya Ufalme wa Mungu.

Sala: Bwana, ninajitoa mwenyewe kwa ajili ya huduma yako na kwa ajili ya utukufu wako. Ninakuomba unitumie mimi niweze kuubadili ulimwengu wetu kuwa sehemu takatifu ya kuishi na sehemu ambayo uzuri wako utatawala. Ninakushukuru kwa upendeleo wa kutumiwa nawe na ninaomba unitumie upendavyo katika kuwa mwanga na chumvi ulimwenguni. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Maoni


Ingia utoe maoni