Ijumaa. 29 Machi. 2024

Tafakari

Jumatano, Septemba 14, 2022

Jumatano, Septemba 14, 2022 
Juma la 24 la Mwaka

Sikukuu ya Kutukuka kwa Msalaba Mtakatifu

Hes 21: 4-9 
Zab 77: 1-2, 34-38
Fil 2: 6-11
Yn 3: 13-17


MSALABA WA KRISTO NI TUMAINI NA UKOMBOZI WETU!

Msalaba ni ishara ya Mkristo. Kila Mkristo, mtoto na hata mtakatifu mkubwa kabisa, wanafanya ishara ya Msalaba, kutoa ushuhuda wa nguvu yake na umuhimu wake. Yesu alitoa maisha yake Msalabani na hapo akakomboa ubinadamu. Kwa njia hii hamna tena alama ya mateso na aibu, bali ukombozi. Msalaba ni njia ya kwenda kwenye utukufu, kwahiyo ni changamoto kwa kila Mkristo. Kama Mtakatfiu Paulo anavyosema “Tunamuhubiri Yesu Msulubiwa, kwa Wayahudi ni kikwazo na kwayunani ni upuuzi, bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani ni Kristo, Nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu” (1 Kor 1: 23-24). 

Katika historia ya Ukristo Msalaba aliofia Kristo na kwa njia hii akafufuka, umekuwa niishara wazi ya nguvu ya Mungu ya kuokoa. Mababa wa Kanisa wanalinganisha Msalaba wa Yesu na mti wa uzima katika bustani ya dunia, safina ya Noah, na kuni alizobeba Isaka katika mlima Moriah, na ile ngazi ya Yakobo, na ile Fimbo ya Musa, na yule nyoka ya Shaba. Haya yote katika hali ya juu yanahusishwa na fumbo la ukombozi. Katika Ubatizo kila Mkristo amesulubiwa na Kristo, kufa na kufufuka na Kristo. Mtakatifu Leo Mkuu anasema, “Msalaba ni chanzo cha kila Baraka, chanzo cha mafanikio yote: kwa waamini unawapa nguvu kutoka katika udhaifu wake, utukufu kutoka katika aibu yake, na uzima kutoka katika kifo”.  

Sala: Ee Msalaba juu ya Ulimwengu, kuwa uponyanji na Ukombozi wangu.

Amina

Maoni


Ingia utoe maoni