Ijumaa. 03 Mei. 2024

Tafakari

Jumanne, Disemba 06, 2016

Jumanne, Desemba 6, 2016,
Juma la 2 la Majilio

Isa 40: 1-11;
Zab 95: 1-3, 10-13;
Mt 18: 12-14


MUNGU ANATAFUTA KONDOO ALIYEPOTEA!

Somo la kwanza kutoka katika kitabu cha nabii Isaya, tunasikia sifa za Mchungaji mwema mwenye huruma na kuwajali kondoo waliopotea (watu wa Israeli). Katika Injili Yesu anatupa mfano wa kondoo aliyepotea. Huyu Mchungaji anawaacha wale tisini na tisa na kwenda kumtafuta aliyepotea. Mfano huu unaendelea na kusema kuwa “atakapo mpata, Amin, nawaambia, atafurahi zaidi juu ya kondoo huyu, kuliko wale tisini na tisa ambao hawakupotea” (Mt 18:13). Huzuni na masikitiko ya huyu Mchungaji yanabadilika na kuwa furaha baada ya kumpata kondoo na kumrudisha kwenye kundi. Kwa haraka haraka inawezekana kuonekana kama sio sawa kwa Mchungaji kumfurahia zaidi huyu aliyepotea baada ya kumpata kuliko wale tisini na tisa. Lakini tukitambua kwamba, kila mmoja wetu ni yule kondoo aliyepotea, ina leta maana zaidi. Tunapotafakari kuhusu mfano huu ni vizuri kufikiria juu ya hamu na tamaa ya huyu Mchungaji na jitihada zake za kututafuta. Hii ndio hali ya Mungu juu yetu. Mungu anatutafuta daima aturudishe kundini mwake.

Tutafakari leo, kuhusu wewe kuwa mmoja wa yule kondoo aliyepotea. Kupotelea kwenye “dhambi” sio jambo linaloleta furaha, dhambi inaleta wasi wasi, maumivu, kukosa Amani, kuchanganyikiwa, hasira na mengine mengi. Lakini tukiinua macho yetu kumwelekea Mchungaji mwema tukiwa katika hali ya dhambi zetu, tutapata tena matumaini mapya. Tutapata matumaini kwamba Mungu wetu anatujali na hachoki kamwe kututafuta. Na anapo tupata moyo wake hujazwa na furaha kuu! Wakati kondoo aliyepotea anapopatikana jumuiya yote ya mbinguni hufurahi. (Lk 15:7).

Sala: Bwana, katikati ya dhambi zangu na kuchanganyikiwa nakurudia. Nina amini kwamba unanitafuta. Ninaomba nijiaminishe kwenye upendo wako wa hali ya juu kwangu. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Maoni


Ingia utoe maoni