Jumanne. 14 Mei. 2024

Masomo ya Misa

Dominika ya 23 ya Mwaka (Jumapili, Septemba 10, 2017)  

Somo la 1

Eze. 33:7-9

Basi wewe, mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi kwa nyumba ya Israeli; basi ulisikie neno hili kinywani mwangu, ukawape maonyo yangu. Nimwambiapo mtu mbaya, Ewe mtu mbaya, hakika utakufa, nawe husemi neno la kumwonya mtu huyo, aiache njia yake, mtu mbaya huyo atakufa katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Walakini ukimwonya mtu mbaya kwa sababu ya njia yake, kusudi aiache; wala yeye asiiache; atakufa huyo katika uovu wake, lakini wewe umejiokoa roho yako.

Wimbo wa Katikati

Zab. 95:1-2, 6-9

Tusifanye migumu mioyo yetu.
Njoni tumwimbie Bwana,
Tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu.
Tuje mbele yake kwa shukrani,
Tumfanyie shangwe kwa zaburi.
(K) Ingekuwa heri leo tusikie sauti yake!

Njoni, tuabudu, tusujudu,
Tupige magoti mbele za Bwana aliyetuumba.
Kwa maana ndiye Mungu wetu,
Na sisi tu watu wa malisho yake,
Na kondoo za mkono wake.
(K) Ingekuwa heri leo tusikie sauti yake!

Ingekuwa heri leo msikie sauti yake!
Msifanye migumu mioyo yenu;
Kama vile huko Meriba;
Kama siku ile ya Masa jangwani,
Hapo waliponijaribu baba zetu;
Wakanipima, wakayaona matendo yangu.
(K) Ingekuwa heri leo tusikie sauti yake!

Somo la 2

Rum. 13:8-10

Msiwiwe na mtu chochote, isipokuwa kupendana; kwa maana ampendaye mwenzake ameitimiza sharia. Maana kule kusema, Usizini, Usiue, Usiibe, Usitamani, na ikiwapo amri nyingine yoyote, inajumlishwa katika neno hili, ya kwamba, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Pendo halimfanyii jirani neno baya, basi pendo ndilo utimilifu wa sheria.

Shangilio

Yn. 14:23

Aleluya, aleluya,
Mtu akinipenda, atalishika neno langu;
Na baba yangu atampenda; Nasi tutakuja kwake.
Aleluya.

Injili

Mt. 18:15-20

Siku ile Yesu aliwaambia wafuasi wake: Ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo. La, kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja au wawili, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike. Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru. Amin, nawaambieni, yoyote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yoyote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni.

Maoni


Ingia utoe maoni