Jumanne. 14 Mei. 2024

Masomo ya Misa

Jumamosi ya 22 ya Mwaka (Jumamosi, Septemba 09, 2017)  

Somo la 1

Kol. 1:21-23

Ninyi, mliokuwa hapo kwanza mmefarikishwa, tena adui katika nia zenu, kwa matendo yenu mabaya, amewapatanisha sasa; katika mwili wa nyama yake, kwa kufa kwake, ili awalete ninyi mbele zake, watakatifu, wasio na mawaa wala lawama; mkidumu tu katika ile Imani, hali mmewekwa juu ya msingi, mkawa imara; msipogeuzwa na kuliacha tumaini la Injili mliyosikia habari zake, iliyohubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu; ambayo mimi Paulo nalikuwa mhudumu wake.

Wimbo wa Katikati

Zab. 54:1-2, 4, 6

Ee Mungu, kwa jina lako uniokoe,
Na kwa uweza wako unifanyie hukumu.
Ee Mungu, uyasikie maombi yangu,
Uyasikie maneno ya kinywa changu.
(K) Mungu ndiye anayenisaidia.

Tazama, Mungu ndiye anayenisaidia
Bwana ndiye anayenitegemeza nafsi yangu,
Kwa ukunjufu wa moyo nitakutolea dhabihu;
Ee Bwana, nitalishukuru jina lako, maana ni jema.
(K) Mungu ndiye anayenisaidia.

Shangilio

Zab. 119:34

Aleluya, aleluya,
Unifahamishe nami nitaishika sheria yako,
nitaitii kwa moyo wangu wote.
Aleluya.

Injili

Lk. 6:1 – 5

Ilikuwa siku ya sabato moja Yesu alikuwa akipita katika mashamba, wanafunzi wake wakawa wakivunja masuke na kuyala, wakiyapukusa-pukusa mikononi mwao. Basi baadhi ya Mafarisayo wakawaambia, Mbona mnafanya lisilo halali siku ya sabato? Yesu akawajibu akawaambia, Hamkulisoma, hata hilo alilolifanya Daudi, alipokuwa na njaa, na yeye na wale aliokuwa nao? Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu, akaitwaa mikate ile ya Wonyesho, akaila akawapa na hao wenziwe, ambayo si halali kuila ila kwa makuhani peke yao. Akawaambia, Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato.

Maoni


Ingia utoe maoni