Jumapili. 12 Mei. 2024

Masomo ya Misa

Kumbukumbu ya Mtakatifu Alfonsi Maria wa Liguori (Jumanne, Agosti 01, 2017)  

Somo la 1

Kut. 33 : 7-11; 34:5-9,28

Desturi ya Musa, ilikuwa kuitwaa ile hema, na kuikita nje ya marago mbali na hayo marago; akaiita, Hema ya kukutania. Hata kila mtu aliyekuwa akitaka neno kwa Bwana, akatoka, akaenda hata hema ya kukutania, iliyokuwa nje ya marago. Hata Musa alipotoka kuiendea ile hema, watu wote waliondoka wakasimama, kila mtu mlangoni pa hema yake, akamtazama Musa, hata alipokwisha kuingia hemani. Ikawa Musa alipoingia humo hemani, ile nguzo ya wingu ikashuka, ikasimama mlangoni pa ile hema; naye Bwana akasema na Musa. Watu wote wakaiona nguzo ya wingu ikisimama penye mlango wa hema; watu wote wakaondoka wakasujudu, kila mtu mlangoni pa hema yake. Naye Bwana akasema na Musa uso kwa uso. kama vile mtu asemavyo na rafiki yake. Kisha akageuka akarejea hata maragoni; bali mtumish wake Yoshua, mwana wa Nuni, naye ni kijana hakutoka mle hemani. Bwana akashuka ndani ya lile wingu, akasimam; pamoja naye huko, akalitangaza jina la Bwana Bwana akapita mbele yake, akatangaza, Bwana Bwana, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu. Mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe; mwenye kuwapatiliza watoto uovu wa baba zao, na wana wa wana wao pia, hata kizazi cha tatu na cha nne. Musa akafanya haraka, akainamisha kichwa chake hata nchi, akasujudu. Akasema, Ikiwa sasa nimepata neema mbele zako, Bwana, nakuomba, Bwana, uende kati yetu, maana ni watu wenye shingo ngumu; ukasamehe uovu wetu na dhambi yetu, ukatutwae tuwe urithi wako. Naye alikuwa pamoja na Bwana siku arobaini na masiku yake; hakula chakula, wala hakunywa maji. Naye akaandika katika hizo mbao, hayo maneno ya maagano. hizo amri kumi.

Wimbo wa Katikati

Zab. 103 : 6-13

Bwana ndiye afanyaye mambo ya haki,
na hukumu kwa wote wanaoonewa.
Alimjulisha Musa njia yake,
wana wa Israeli matendo yake.
(K) Bwana amejaa huruma na neema.

Bwana amejaa huruma na neema,
haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili.
Yeye hatateta sikuzote,
wala hatashika hasira yake milele.
(K) Bwana amejaa huruma na neema.

Hakututenda sawasawa na hatia zetu,
wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu.
Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi,
kadiri ileile rehema zake ni kuu kwa wamchao.
(K) Bwana amejaa huruma na neema.

Shangilio

2Tim 1:10

Aleluya, aleluya,
Mwokozi wetu Yesu Kristu alibatili mauti,
na kuufunua uzima na kutokuharibika kwa Injili.
Aleluya.

Injili

Mt. 13 :36-43

Yesu aliwaaga makutano, akaingia nyumbani; wanafunzi wake wakamwendea, wakasema, Tufafanulie mfano wa magugu ya kondeni. Akajibu, akasema, Azipandaye zile mbegu njema ni Mwana wa Adamu; lile konde ni ulimwengu; zile mbegu njema ni wana wa ufalme; na yale magugu ni wana wa yule mwovu; yule adui aliyeyapanda ni Ibilisi; mavuno ni mwisho wa dunia; na wale wavunao ni malaika. Basi, kama vile magugu yakusanywavyo na kuchomwa motoni; ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia. Mwana wa Adamu atawatuma malaika zake, nao watakusanya kutoka katika ufalme wake machukizo yote, na hao watendao maasi, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. Ndipo wenye haki watakapong’aa kama jua katika ufalme wa Baba yao. Mwenye masikio, na asikie.

Maoni


Ingia utoe maoni