Alhamisi. 19 Septemba. 2024

Masomo ya Misa

(Jumatano, Januari 13, 2016)  

Somo la 1

1Sam. 3:1-10, 19-20

Mtoto Samweli alimtumikia Bwana mbele ya Eli. Na neno la Bwana lilikuwa adimu siku zile; hapakuwa na mafunuo Dhahiri. Ikawa wakati huo, Eli alipokuwa amelala mahali pake (tena macho yake yalikuwa yameanza kupofuka, hata asiweze kuona, na taa ya Mungu ilikuwa haijazimika bado, na Samweli alikuwa amelala katika hekalu la Bwana, palipokuwa na sanduku la Mungu; basi, wakati huo Bwana akamwita Samweli; naye akasema, Mimi hapa. Akamwendea Eli kwa haraka, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Akasema, Sikukuita; kalale tena. Naye akaenda, akalala tena. Bwana akaita mara ya pili, Samweli! Samweli! Akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Akajibu, Sikukuita, mwanangu; kalale tena. Basi Samweli alikuwa hamjui Bwana bado, na neno la Bwana lilikuwa bado halijafunuliwa kwake. Bwana akamwita Samweli mara ya tatu. Naye akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Ndipo Eli akatambua ya kuwa Bwana ndiye aliyemwita yule mtoto. Kwa hiyo Eli akamwambia Samweli, Enenda kalale; itakuwa akikuita, utasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia. Basi Samweli akaenda akalala mahali pake. Bwana akaja, akasimama, akaita vile vile kama kwanza, Samweli! Samweli! Ndipo Samweli akasema Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia. Samweli akakua, naye Bwana alikuwa pamoja naye, wala hakuliacha neno lake lolote lianguke chini. Nao Waisraeli wote, toka Dani mpaka Beersheba, walitambua ya kwamba huyo Samweli amewekwa kuwa nabii wa Bwana.

Wimbo wa Katikati

Zab. 40:1,4,6-9

Nalimngoja Bwana kwa saburi,
Akaniinamia akakisikia kilio changu.
Heri aliyemfanya Bwana kuwa tumaini lake,
Wala hakuwaelekea wenye kiburi,
Wala hao wanaogeukia uongo.

Dhabihu na matoleo hukupendezwa nazo,
Masikio yangu umeyazibua,
Kafara na sadaka za dhambi hukuzitaka.
Ndipo niliposema, Tazama nimekuja.

Katika gombo la chuo imeandikwa,
Kuyafanya mapenzi yako,
Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu,
Naam, sheria yako imo moyoni mwangu.

Nimehubiri habari za haki katika kusanyiko kubwa,
Sikuizuia midomo yangu, Ee Bwana, unajua.

Injili

Mk. 1:29-39

Siku ile, Yesu alipotoka katika sinagogi, walifika nyumbani kwa Simoni na Andrea, pamoja na Yakobo na Yohane. Naye mkewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa kitandani, hawezi homa; na mara wakamwambia habari zake. Akamkaribia, akamwinua kwa kumshika mkono, homa ikamwacha, akawatumikia. Hata kulipokuwa jioni, na jua limekwisha kuchwa, walikuwa wakimletea wote waliokuwa hawawezi, na wenye pepo. Na mji wote ulikuwa umekusanyika mlangoni. Akaponya wengi waliokuwa na maradhi mbalimbali, akatoa pepo wengi, wala hakuwaacha pepo kunena, kwa sababu walimjua. Hata alfajiri na mapema sana akaondoka, akatoka akaenda zake mahali pasipokuwa na watu, akaomba huko. Simoni na wenziwe wakamfuata; nao walipomwona wakamwambia, Watu wote wanakutafuta. Akawaambia, Twendeni mahali pengine, mpaka vijiji vilivyo karibu, nipate kuhubiri huko nako; maana kwa hiyo nalitokea. Akaenda akihubiri katika masinagogi yao, katika nchi yote ya Galilaya, na kutoa pepo.

Maoni


Ingia utoe maoni