Alhamisi. 30 Julai. 2026

Masomo ya Misa

Kumbukuku ya Mtakatifu Martha (Jumatano, Julai 29, 2026)  

Somo la 1

Yer 15:10, 16-21

Ole wangu, mama yangu, kwa kuwa umenizaa mtu wa kuteta, na mtu wa kushindana na dunia yote! Mimi sikukopesha kwa riba, wala watu hawakunikopesha kwa riba; lakini kila mmoja wao hunilaani. Maneno yako yalionekana, nami nikayala; na maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu, na shangwe ya moyo wangu; maana nimeitwa kwa jina lako, Ee Bwana, Mungu wa majeshi. Sikuketi katika mkutano wao wanaojifurahisha, wala sikufurahi, naliketi peke yangu kwa sababu ya mkono wako; kwa maana umenijaza ghadhabu. Mbona maumivu yangu ni ya daima, na jeraha yangu haina dawa, inakataa kuponywa? Je! Yamkini wewe utakuwa kwangu kama kijito kidanganyacho, na kama maji yasiyodumu? Kwa sababu hiyo Bwana asema hivi, Ukirudi, ndipo mimi nitakapokurejeza, upate kusimama mbele zangu; nawe ukitoa kilicho cha thamani katika kilicho kibovu, utakuwa kama kinywa changu; nao watakurudia wewe, bali hutawarudia wao. Nami nitakufanya kuwa kama ukuta wa boma la shaba juu ya watu hawa; nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, ili nikuokoe, na kukuponya, asema Bwana. Nami nitakuokoa na mkono wa watu wabaya, nami nitakukomboa katika mkono wao wenye kutisha.

Wimbo wa Katikati

Zab 59:2-4, 10-11, 17-18

Ee Mungu wangu, uniponye na adui zangu, Uniinue juu yao wanaoshindana nami.
Uniponye nao wafanyao maovu, Uniokoe na watu wa damu.
(K) Bwana alikuwa ngome yangu siku ya shida yangu

Kwa maana wanaiotea nafsi yangu; Wenye nguvu wamenikusanyikia;
Ee Bwana, si kwa kosa langu, Wala si kwa hatia yangu.
(K) Bwana alikuwa ngome yangu siku ya shida yangu

Ee nguvu zangu, nitakungoja Wewe, Maana Mungu ndiye aliye ngome yangu
Mungu wa fadhili zangu atanitangulia, Mungu atanijalia kuwatazama adui zangu.
(K) Bwana alikuwa ngome yangu siku ya shida yangu

Nami nitaziimba nguvu zako asubuhi, Nitaziimba fadhili zako kwa furaha.
Kwa kuwa ndiwe uliyekuwa ngome yangu, Na makimbilio siku ya shida yangu.
(K) Bwana alikuwa ngome yangu siku ya shida yangu

Ee nguvu zangu, nitakuimbia kwa furaha,
Maana Mungu ndiye aliye ngome yangu, Mungu wa fadhili zangu.
(K) Bwana alikuwa ngome yangu siku ya shida yangu

Shangilio

Yak 1:21

Aleluya, aleluya,
Pokeeni kwa upole neno la Mungu lililopandwa ndani, liwezalo kuziokoa roho zenu.
Aleluya.

Injili

Yn 11:19-27

Watu wengi katika Wayahudi walikuwa wamekuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa habari ya ndugu yao. Basi Martha aliposikia kwamba Yesu anakuja, alikwenda kumlaki; na Mariamu alikuwa akikaa nyumbani. Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa. Yesu akamwambia, Ndugu yako atafufuka. Martha akamwambia, Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho. Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo? Akamwambia, Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni.

Maoni


Ingia utoe maoni