Jumapili. 05 Mei. 2024

Masomo ya Misa

SHEREHE YA MARIA MTAKATIFU MAMA WA MUNGU (Jumapili, Januari 01, 2017)  

Somo la 1

Hes. 6:22-27

Bwana akanena na Musa, na kumwambia, Nena na Haruni na wanawe, uwaambie, Hivi ndivyo mtakavyowabarikia wana wa Israeli; mtawaambia; Bwana akubarikie, na kukulinda; Bwana akuangazie nuru za uso wake, na kukufadhili; Bwana akuinulie uso wake, na kukupa Amani. Ndivyo watakavyoweka jina langu juu ya wana wa Israeli; nami nitawabarikia.

Wimbo wa Katikati

Zab. 67:1-2,4,6-7

Mungu na atufadhili na kutubariki,
Na kutuangazia uso wake.
Njia yake ijulikane duniani,
Wokovu wake katikati ya mataifa yote.
(K) Mungu na atufadhili na kutubariki.


Mataifa na washangilie,
Naam, waimbe kwa furaha,
Maana kwa haki utawahukumu watu,
Na kuwaongoza mataifa walioko duniani.
(K) Mungu na atufadhili na kutubariki.


Nchi imetoa mazao yake;
Mungu, Mungu wetu, ametubariki.
Mungu atatubariki sisi;
Miisho yote ya dunia itamcha Yeye.
(K) Mungu na atufadhili na kutubariki.

Somo la 2

Gal. 4:4-7

Ndugu zangu: ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana. Na kwa kuwa ninyi mmekuwa wana. Mungu alimtuma Roho wa Mwanawe mioyoni mwetu, aliaye, Aba, yaani, Baba. Kama ni hivyo, wewe si mtumwa tena bali u mwana na kama u mwana, basi, u mrithi kwa Mungu.

Injili

Lk. 2:16-21

Siku ile: Wachungaji wakaenda kwa haraka wakamkuta Mariamu na Yusufu, na yule mtoto mchanga amelala horini. Walipomwona wakatoa habari waliyoambiwa juu ya huyo mtoto. Wote waliosikia wakastaajabu kwa hayo waliyoambiwa na wachungaji. Lakini Mariamu akayaweka maneno hayo yote, akiyafikiri moyoni mwake. Wale wachungaji wakarudi, huku wanamtukuza Mungu na kumsifu kwa mambo yote waliyosikia na kuyaona, kama walivyoambiwa. Hata zilipotimia siku nane za kumtahiri, aliitwa jina lake Yesu; kama alivyoitwa na malaika kabla hajachukuliwa mimba.

Maoni


Ingia utoe maoni