Ijumaa. 03 Mei. 2024

Masomo ya Misa

Ijumaa ya 2 ya Majilio (Ijumaa, Desemba 09, 2016)  

Somo la 1

Isa 48:17-19

Bwana, mkombozi wako, mtakatifu wa Israeli, asema hivi; Mimi ni Bwana, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata. Laiti ungalisikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari; Tena wazao wako wangalikuwa kama mchanga, na hao waliotoka katika tumbo lako kama chembe zake; jina lake lisingalikatika, wala kufutwa mbele zangu.

Wimbo wa Katikati

Zab 1:1-4, 6

Heri mtu yule asiyekwenda Katika shauri la wasio haki;
Wala hakusimama katika njia ya wakosaji;
Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha.
Bali sheria ya Bwana ndiyo impendezayo,
Na sheria yake huitafakari mchana na usiku.
(K) Akufuataye, Bwana, atakuwa na nuru ya uzima.

Naye atakuwa kama mti uliopandwa Kandokando ya vijito vya maji,
Uzaao matunda yake kwa majira yake, Wala jani lake halinyauki;
Na kila alitendalo litafanikiwa.
(K) Akufuataye, Bwana, atakuwa na nuru ya uzima.

Sivyo walivyo wasio haki; Hao ni kama makapi yapeperushwayo na upepo.
Kwa kuwa Bwana anaijua njia ya wenye haki,
Bali njia ya wasio haki itapotea.
(K) Akufuataye, Bwana, atakuwa na nuru ya uzima.

Shangilio

Shangilio

Aleluya, aleluya,
Bwana atakuja, nendeni kumlaki, Yeye ni mfalme wa Amani.
Aleluya.

Injili

Mt 11:16-19

Yesu aliwaambia makutano: Lakini nitakifananisha na nini kizazi hiki? Kimefanana na watoto wanaokaa sokoni, wanaowaita wenzao, wakisema, Tuliwapigia filimbi, wala hamkucheza; tuliomboleza, wala hamkulia. Maana Yohana alikuja, hali wala hanywi, wakasema, Yuna pepo. Mwana wa Adamu alikuja, akila na kunywa, wakasema, Mlafi huyu, na mlevi, rafiki yao watoza ushuru na wenye dhambi! Na hekima imejulikana kuwa ina haki kwa kazi zake.

Maoni


Ingia utoe maoni