Jumapili. 08 Septemba. 2024

Masomo ya Misa

Jumatano ya 16 ya Mwaka C (Jumatano, Julai 24, 2024)  

Somo la 1

Yer 1:1, 4-10

Maneno ya Yeremia, mwana wa Hilkia, mmoja wa makuhani waliokuwa katika Anathothi, katika nchi ya Benyamini; Neno la Bwana lilinijia, kusema, Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa. Ndipo niliposema, Aa, Bwana MUNGU! Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto. Lakini Bwana akaniambia, Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru. Usiogope kwa sababu ya hao maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe, asema Bwana. Ndipo Bwana akaunyosha mkono wake, akanigusa kinywa changu; Bwana akaniambia, Tazama, nimetia maneno yangu kinywani mwako; angalia, nimekuweka leo juu ya mataifa na juu ya falme, ili kung'oa, na kubomoa, na kuharibu, na kuangamiza; ili kujenga na kupanda.

Wimbo wa Katikati

Zab 71:1-6, 15, 17

Nimekukimbilia Wewe, Bwana, Nisiaibike milele.
Kwa haki yako uniponye, uniopoe, Unitegee sikio lako, uniokoe.
(K) Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako.

Uwe kwangu mwamba wa makazi yangu, Nitakakokwenda sikuzote. Umeamuru niokolewe, Ndiwe genge langu na ngome yangu.
Ee Mungu wangu, uniopoe mkononi mwa mkorofi, Katika mkono wake mwovu, mdhalimu,
(K) Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako.

Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU, Tumaini langu tokea ujana wangu.
Nimekutegemea Wewe tangu kuzaliwa, Ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu, Ninakusifu Wewe daima.
(K) Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako.

Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako Mchana kutwa; maana sijui hesabu yake.
Ee Mungu, umenifundisha tokea ujana wangu; Nimekuwa nikitangaza miujiza yako hata leo.
(K) Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako.

Shangilio

.

Aleluya, aleluya
Neno la Mungu ni mbegu, na Kristu ndiye mpanzi, wote watakaokuja kwake wataishi milele.
Aleluya

Injili

Mt 13:1-9

Yesu alitoka nyumbani, akaketi kando ya bahari. Wakamkusanyikia makutano mengi, hata akapanda chomboni, akaketi; na ule mkutano wote wakasimama pwani. Akawaambia mambo mengi kwa mifano, akisema, Tazama, mpanzi alitoka kwenda kupanda. Hata alipokuwa akipanda, mbegu nyingine zilianguka karibu na njia, ndege wakaja wakazila; nyingine zikaanguka penye miamba, pasipokuwa na udongo mwingi; mara zikaota, kwa udongo kukosa kina; na jua lilipozuka ziliungua; na kwa kuwa hazina mizizi zikanyauka. Nyingine zikaanguka penye miiba; ile miiba ikamea, ikazisonga; nyingine zikaanguka penye udongo mzuri, zikazaa, moja mia, moja sitini, moja thelathini. Mwenye masikio na asikie.

Maoni


Ingia utoe maoni