Jumatatu. 06 Mei. 2024

Masomo ya Misa

Jumanne ya 3 ya Pasaka (Jumanne, Aprili 16, 2024)  

Somo la 1

Mdo 7:51-8:1

Stefano aliwaambia Wakuu wa Makuhani: Enyi wenye shingo gumu, msiotahiriwa mioyo wala masikio, sikuzote mnampinga Roho Mtakatifu; kama baba zenu walivyofanya, na ninyi ni vivyo hivyo. Ni yupi katika manabii ambaye baba zenu hawakumwudhi? Nao waliwaua wale waliotabiri habari za kuja kwake yule Mwenye Haki; ambaye ninyi sasa mmekuwa wasaliti wake, mkamwua; ninyi mlioipokea torati agizo la malaika msiishike. Basi waliposikia maneno haya, wakachomwa mioyo, wakamsagia meno. Lakini yeye akijaa Roho Mtakatifu, akakaza macho yake, akitazama mbinguni, akauona utukufu wa Mungu, na Yesu akisimama upande wa mkono wa kuume wa Mungu. Akasema, Tazama, naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu. Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli. Wakampiga kw amawe Stefano, naye akiomba, akisema Bwana Yesu, pokea roho yangu. Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.

Wimbo wa Katikati

Zab 31:2-3, 5, 7, 16, 20

Uwe kwangu mwamba wa nguvu,
Nyumba yenye maboma ya kunionkoa.
Ndiwe genge langu na ngome yangu;
Kwa ajili ya jina lako uniongoze, unichunge.
(K) Mikononi mwako naiweka roho yangu, ee Bwana.

Mikononi mwako naiweka roho yangu;
Umenikomboa, Ee Bwana, Mungu wa kweli.
Bali mimi namtumaini Bwana.
Na nishangilie, nizifurahie fadhili zako.
(K) Mikononi mwako naiweka roho yangu, ee Bwana.

Umwangaze mtumishi wako,
Kwa nuru ya uso wako;
Uniokoe kwa ajili ya fadhili zako.
Utawaficha katika hema
Na mashindano ya ndimi.
(K) Mikononi mwako naiweka roho yangu, ee Bwana.

Shangilio

Yn 10:14

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi mchungaji mwema, nao walio wangu nawajua, nao walio wangu wanijua mimi.
Aleluya.

Injili

Yn 6:30-35

Siku ile, Wayahudi walimwambia Yesu: Unafanya ishara gani basi, ili tuione tukakuamini? Unatenda kazi gani? Baba zetu waliila mana jangwani, kama vile ilivyoandikwa, Aliwapa chakula cha mbinguni ili wale. Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Siye Musa aliyewapa chakula kile cha mbinguni, bali Baba yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni. Kwa maana chakula cha Mungu ni kile kishukacho kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima. Basi wakamwambia, Bwana, sikuzote utupe chakula hiki. Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe.

Maoni

Martin Muteti

Amina

Ingia utoe maoni